Sababu 8 za Wanaume Kutokuwa Waaminifu Katika Mahusiano Yao ya Mapenzi - NYUMBA YA MAPENZI

Breaking

Sunday, February 24, 2019

Sababu 8 za Wanaume Kutokuwa Waaminifu Katika Mahusiano Yao ya Mapenzi


Suala la wanandoa kutokuwa waaminifu kwenye mahusiano yao ni suala mtambuka na limekuwa likiongelewa sana na watu wengi. Sababu mablimbali zimekuwa zikitajwa kuwa chanzo, nyingine ni za kweli na nyingine ni zakufikirika tu.

Leo nimeamua kuja na sababu zinazotokana na tafiti za wanaume kutokuwa waaminifu kwenye mahusiano na ndoa. Ikumbukwe kwamba sababu za wanawake kutokuwa waaminifu hazifanani moja kwa moja na sababu za wanaume, na hata kitendo chakutokuwa mwaminifu kwenye ndoa kwa mume au mke pia huathiri ndoa husika katika uzito tofauti. Hii ni kutokana na sababu za kiasilia, kiuumbaji, kijinsia na kisaikolojia.


Sababu:

1. Utupu au upweke ndani ya moyo wa mwanaume

Pamoja na kwamba wanaume huonekana wakiwa jasiri sana kwa nje ila ieleweke kwamba ni viumbe dhaifu ndani, ni viumbe wasioweza kuvumilia upweke ndani yao, wakati wote hutamani kuwa karibu na mwanamke hata kama akiwepo karibu hawaelewani mara kwa mara. Maranyingi kwenye mahusiano unakuta mwanaume ameoa au ana mpenzi na kuna mambo yanaendelea ambayo yanasumbua mahusiano yao, ukaribu unapokosekama mwanaume huanza kujihisi upweke ndani yake na hapo inanyanyuka kiu ya kutafuta mtu wakuondoa upweke ule.

Inasemekana kwamba wanaume wengi huchepuka au kuanza mchakato wa kuchepuka kunapokuwa na tafrani kwenye mapenzi au ndoa, ni kwanini? Sababu ni kwamba ule ugomvi umeleta baridi moyoni na nafsini kwa mwanaume na hawezi kustahimili upweke huo ndani yake kwahiyo anatafuta faraja haraka sana.

Ndio maana tafiti zinaonyesha mara nyingi kwamba mke anapofiwa na mumewe, mke anaweza kuishi muda mrefu bila ya mume na asiolewe, ila mume hawezi kuishi muda mrefu bila kuoa na wale wanaoishi bila mke tena maranyingi hufariki sio muda mrefu.

Ndio maana ulimwengu una wajane wengi kuliko wagane (wanaume waliopoteza wake zao). Ili kupunguza athari za mwanaume kutokuwa mwaminifu ninashauri wanandoa kuhakikisha ukaribu baina yao “intimacy” ni mkubwa na wanaukoleza kwa makusudi kila mara ili kuiepusha ndoa yao kuingia kwenye misukosuko ya kukosekana kwa uaminifu “cheating”

2. Uasili wa kiu kubwa ya mwanaume katika tendo la ndoa

Kiaasili na kibaiolojia mwanaume anakiu kubwa na utayari wa kufanya tendo la ndoa mara kwa mara, mwanaume wa kawaida anaweza kutamani kufanya tendo la ndoa hata kila siku, na wengine hata marambili kwa siku kama kila kitu akilini na katika afya yake ni sawa. Utayari na uwezo huu ni tofauti sana kulinganisha na wanawake ambao kama akifanya tendo zuri la ndoa na hamu yake ikitoshelezwa basi anaweza kukaa muda fulani bila kutamani tena.

Mwanaume hajaumbwa hivyo na wala hawezi. Kwa bahati mbaya kwenye ndoa nyingi wanandoa hawafundishwi haya kwahiyo hawafahamiani asili zao, mwanamke anadhania kuwa atafanya tendo la ndoa anavyotamani yeye kumbe mume aliyenaye ni kiumbe mwingine wa tofauti sana anatamani kupewa tendo hilo kila mara, kwa kutokutosheka mwanaume analazimika kupenya kwenye kona nyinginezo na kupata anachotamani.

Kwa ndoa ya kawaida, mwanamke analazimika kufanya tendo landoa katika nyakati anazotamani na kujisikia na hata zile ambazo atafanya tu ili kumfurahisha na kumsaidia mumewe kufurahi na ndio maana kuna tendo la ndoa la aina mbili kwenye ndoa, tendo la ndoa wakati wote mnafuraha na hamasa na mnajisikia “pleasure s3x” na tendo la ndoa wakati mmoja au wote hamko kwenye hamasa lakini mnalazimika kufanya kwasababu ya uhitaji wa mmoja au usalama wa ndoa yenu “duty s3x”.

3. Kubadilika kwa uzuri, urembo na maumbile ya mke


Mara nyingi ninapoongea na wanawake huwa ninawaambia kwamba mume wako anakupenda uwe vile alivyokupenda alipokutana nawewe, mabadiliko yoyote ya ziada kutoka kwenye ile hali iliyompa hamasa awali yanaweza kuigharimu ndoa yako. Wanaume ni watu wenye kuhamaki au kuwa makini kwenye umbo, umbile na muonekano wa mpenzi wake kwasababu kwa asili mwanaume huvutiwa zaidi na akionacho, mwanaume hufungulia milango ya hisia inayohusu tendo la ndoa kupitia anachokiona zaidi kuliko vitu vingine vyote.

Wanaume wengi waliohojiwa wameripoti mwamba wamepoteza mvuto kwa wake zao kwasababu wake hao wameongezeka maumbo, wamekuwa wanene sana, tumbo limeongezeka, kiuno kimeongezeka, wengine wamesema kwamba uzito na ukubwa wa mwili unawafanya wanawake hawa kutokuwajibika ipasavyo wanapokuwa kitandani, mume anaona kama anadhulumiwa, anakosa ile hamasa aliyoizoea kwenye tendo la ndoa, anakosa ule ushirikiano na uwajibikaji aliouzoea na anaoupenda.

Kumbuka kwamba tendo la ndoa ndio kitovu cha furaha ya mwanaume kwahiyo mabadiliko yoyote yanayoathiri tendo hilo ni hatari sana kwake. Ushauri wangu kwa wanawake, msidharau hoja za waume zenu kuhusu miili yenu, ukisikia anakwambia fanya mazoezi, au anakwambia umeongezeka sana, tafadhali sana zingatia na wala usichukie wala kuhamaki au kuhisi kuwa anatania, kwake huo ni ujumbe muhimu sana. Na wale ambao waume zenu ni wakimya na hawaongei basi fahamu kuwa ndani yake kunakitu kinasugua akili kuhusu kuongezeka kwako, jaribu kufanya kitu kukusaidia kurudi ulivyokuwa awali. Yeye anapenda na inamfurahisha hata kama hasemi.


4. Kuchangamkia fursa ya kupata tendo la ndoa jepesi

Kwasababu wanaume ni watu wanaopenda tendo la ndoa mara kwa mara, na kwasababu wake zao hawako tayari kutimiza kiu hii mara kwa mara kulingana na uhitaji, wanaume wengi huchangamkia fursa pale wanapokutana na uwezekano wakupata tendo la ndoa kirahisi na kiwepesi.

Hii huongezeka zaidi pale ambapo kuna misuguano ndani ya nyumba na kwahiyo wanandoa hawawezi kuweka hisia na mawazo yao katika tendo la ndoa, mume hatakama anakiu kiasi gani anawaza anamuanzaje mkewe, maana anajua fika kwamba atakataliwa, wengine kutokana na ukaribu “intimacy” baina yao kuwa mbaya, mwanaume anaona ugumu kumtongoza mkewe ampe tendo la ndoa, akiwaza kuanza mchakato huu anaona nijukumu zito kama kujenga nyumba, sasa mtu wa hivi anapopata fursa rahisi na nyepesi kutoka kwa kiumbe yeyote wa kike ukweli ni kwamba hatoiacha.

Hapa ndipo panapochochea biashara ya umalaya, kwasababu mwanaume anaona ngoja nitumie shilingi elfu tano au kumi au ishirini ilimalizane nahii hamu maramoja nirudi nyumbani. Ndio maana pia wanawake waliorahisi au wanaojirahisisha kingono hutumiwa sana na wanaume hususani na waume za watu maana kiu yao ni kuitumia fursa hiyo kiufasaha na kuondoka “no strings attached”.


5. Kisasi “revenge”

Mara nyingi wanaume hutumia kitendo cha kutoka nje ya ndoa au nje ya mahusiano kama fimbo ya kulipiza kisasi kwa maumivu au hasira yoyote aliyokuwa nayo dhidi ya mpenzi au mke wake. Kwa mfano, wanaume wengi nilioongea nao binafsi, hususani wale ambao walikuwa wanalalamika kuwa mke wangu haniheshimu, mke wangu ananidharau, mke wangu hanisikilizi, mke wangu anafanya hivi au anafanya vile, wengi baada ya kuongea au kulalamika kwa muda mrefu pasipo kuona mabadiliko baadaye waliamua kuanza ku “cheat”.
Kisaikolojia, mwanaume anapochepuka kwa sababu ya kisasi, huwa inamwondolea ile hali ya kujishtaki au kushtakiwa nafsini kwamba amefanya kosa “guilty conscious” na hiyo inaweza kumfanya aendelee kuchepuka kwa muda mrefu tu, tofauti na mwanamke anapochepuka.

Ni vema ukachukua tahadhari hii, pale unapoona mume wako analalamika sana kuwa haumuheshimu, unamdharau, haumsikilizi, haushuki au kunyenyekea basi fahamu kwamba kunauwezekano mkubwa ameshaanza kuchepuka au yuko kwenye kuisoma ramani ili aanze. Kama kunauwezekano wa kubadili tabia na kushuhulikia hayo malalamiko yake ni bora ukafanya hivyo maana kifuatacho chaweza kuhatarisha mahusiano yenu.


6. Mkanganyiko wa matarajio ya mwanaume

Wako wanaume wengi ambao kabla hawajaoa walikuwa na shauku kubwa kwa wake zao, walikuwa na matamanio au matarajio makubwa kwa wake zao. Wengine walioa wake zao kwasababu ya maumbo mazuri na yakuvutia, wengine ni aina ya familia wanawake hao walizotoka, wengine walioa wakitegemea huyu mwanamke ni mcha Mungu sana, au uliwahi kusikia habari zake nzuri kwa watu na ukatamani sana kuwa naye maishani na mara baada ya kuingia kwenye ndoa bahati mbaya yale mambo uliyokuwa unakiu nayo sana na kuyatarajia unakuta sio yalivyo. Wapo ambao nimeongea nao sana, wanasema walipooa lile umbo zuri sana la mke wake alidhania ndio ustadi wa kitandani baadaye akakuta ujuzi wa tendo la ndoa ni mdogo kuliko matarajio ya mwanaume.

Wengine baada ya ndoa wamekuja kugundua tabia zilizojificha kwa mke ambazo hawakuzijua awali, wengine wameibua madhaifu kedekede kwa wake zao ambayo mwanzoni hawakuyafikiria. Hii hali ya matarajio ya mwanaume kufukiwa na uhalisia huua kabisa hamasa ya tendo la ndoa na hapo inakuwa rahisi mwanaume kuanza kutafuta mahusiano mengine nje.


 7. Kutokupevuka

Wapo wanaume kwenye ndoa hususani wenye umri usio mkubwa sana wamekuwa wakiripotiwa kuchepuka mara kwamara kwasababu tubado hawajafahamu umuhimu wa ndoa ili kuithamini, wameoa lakini bado fikra zao zinatawaliwa na marafiki, hawawezi kujisimamia wenyewe, mtu anaweza kukaa baa na marafiki hadi usiku sana bila kujali kwamba ana mke na watoto. Huko nje usiku ndipo fursa za uchepukaji huzaliwa. Wapo ambao wamechelewa kupevuka kutokana na aina ya malezi waliyolelewa na wazazi wao “spoilt children”, hawa hushindwa kuiheshimu ndoa na mke hatakama mke alalamike vipi.

Kila siku kesi ni kuhusu michepuko, simu imekutwa na picha za ngono za mwanamke, simu ina ujumbe wa mapenzi na vingine vingi vinavyofanana na hivi. Baadhi ya ndoa za wanaume wa hivi zimevunjika mapema kwasababu wake zao walishindwa kustahimili. Kupevuka hakuangalii sana umri, mwanaume anaweza kuwa na umri wa miaka 40 lakini bado haonyeshi kupevuka. Kupevuka ni kukua au kupanuka kwa uwezo wa kufikiri hususani katika kuithamini na kuiheshimu familia, mke  na ndoa kwa ujumla.


8. Kujifariji kwamba kila mtu anafanya

Wapo wanaume wengi walioonyesha kuchepuka kwasababu tu ndani yao walikuwa wanakosa umaana wa kuwa waaminifu kwasababu wanaona hata wale watu ambao wao waliwaamini kwamba labda wanaweza kutochepuka na wao pia walichepuka, sasa mtu anasema kumbe kila mwanaume anachepuka, basi yanini kujibanabana wakati namimi ninahamu na fursa inaruhusu.

Kile kitendo chakuona wanaume wengi wanatabia ya kutokuwa waaminifu kudhoofisha mioyo ya wanaume wengine kwa kujifariji kwamba kumbe hichikitu sio kipya, kila mtu anakijua na anafanya, chakujitahidi tu ni kutokugundulika. Pamoja na hayo wito wangu kwa wanaume wenye fikra hizi ni kwamba, kuwa kwako mwaminifu kwa ndoa yako hakutakiwi kuyumbishwa na tabia za wengine, usimtegemee mtu kukutengenezea misingi ya uaminifu wa ndoa yako, je kama kila mwanaume anampiga mke wake na wewe ndio uanze kumpiga? Kama kila familia inaugomvi, na wewe ndio utafute ugomvi hata kama hakuna mazingira ya ugomvi? La hasha!!

Ifahamike kwamba, haijalishi ni sababu gani imemfanya mwanaume au mwanamke kuchepuka au kukosa uaminifu katika ndoa yake, madhara ya tabia hii yanaweza kuigharimu ndoa yako kwa kiasi kikubwa sana. Madhara yake yanaweza pia yasiishie kwenu ninyi wanandoa tu bali yakawaathiri hata watoto wenu. Wito wangu ni kila mwanandoa kuithamini na kuiheshimu ndoa yake kutoka ndani yamoyo na sio kinafiki.


Usisahau kushare post hii.👍 Share facebook, twitter, Google+ n.k bila kusahau WhatsApp! Share kote wenzio nao wasome

No comments:

Post a Comment